Translations Suras
KISWAHILI

90 - AL - BALAD

KWA JINA LA MWENYEZI MUNGU MWINGI WA REHEMA MWENYE KUREHEMU.

 
1Naapa kwa Mji huu!
 
2Nawe unaukaa Mji huu.
 
3Na naapa kwa mzazi na alicho kizaa.
 
4Hakika tumemuumba mtu katika taabu.
 
5Ati anadhani hapana yeyote ataye muweza?
 
6Anasema: Nimeteketeza chungu ya mali.
 
7Ati anadhani ya kuwa hapana yeyote anaye mwona?
 
8Kwani hatukumpa macho mawili?
 
9Na ulimi, na midomo miwili?
 
10Na tukambainishia zote njia mbili?
 
11Lakini hakujitoma kwenye njia ya vikwazo vya milimani.
 
12Na nini kitakujuvya ni nini njia ya vikwazo vya milimani?
 
13Kumkomboa mtumwa;
 
14Au kumlisha siku ya njaa
 
15Yatima aliye jamaa,
 
16Au masikini aliye vumbini.
 
17Tena awe miongoni mwa walio amini na wakausiana kusubiri na wakausiana kuhurumiana.
 
18Hao ndio watu wa kheri wa kuliani.
 
19Lakini walio zikataa Ishara zetu, hao ndio watu wa shari wa kushotoni.
 
20Juu yao utakuwa Moto ulio fungiwa kila upande.
 
 
ReadTheQuran.org