Translations Suras
KISWAHILI

78 - ANNABAA

KWA JINA LA MWENYEZI MUNGU MWINGI WA REHEMA MWENYE KUREHEMU.

 
1WANAULIZANA nini?
 
2Ile khabari kuu,
 
3Ambayo kwayo wanakhitalifiana.
 
4La! Karibu watakuja jua.
 
5Tena la! Karibu watakuja jua.
 
6Kwani hatukuifanya ardhi kama tandiko?
 
7Na milima kama vigingi?
 
8Na tukakuumbeni kwa jozi?
 
9Na tukakufanya kulala kwenu ni mapumziko?
 
10Na tukaufanya usiku ni nguo?
 
11Na tukaufanya mchana ni wa kuchumia maisha?
 
12Na tukajenga juu yenu saba zenye nguvu?
 
13Na tukaifanya taa yenye mwanga na joto;
 
14Na tukateremsha maji yanayo anguka kwa kasi kutoka mawinguni,
 
15Ili tutoe kwayo nafaka na mimea,
 
16Na mabustani yenye miti iliyo kamatana.
 
17Hakika siku ya uamuzi imewekewa wakati wake,
 
18Siku litapo pulizwa barugumu, nanyi mtakuja kwa makundi,
 
19Na mbingu zitafunguliwa, ziwe milango,
 
20Na milima itaondolewa na itakuwa kama sarabi.
 
21Hakika Jahannamu inangojea!
 
22Kwa walio asi ndio makaazi yao,
 
23Wakae humo karne baada ya karne,
 
24Hawataonja humo chochote kibaridi wala kinywaji,
 
25Ila maji yamoto sana na usaha,
 
26Ndio jaza muwafaka.
 
27Hakika hao hawakuwa wakitaraji kuwa kuna hisabu.
 
28Na wakikanusha Aya zetu kwa nguvu.
 
29Na kila kitu Sisi tumekidhibiti kwa kukiandika.
 
30Basi onjeni! Nasi hatutakuzidishieni ila adhabu!
 
31Hakika wachamngu wanastahiki kufuzu,
 
32Mabustani na mizabibu,
 
33Na wake walio lingana nao,
 
34Na bilauri zilizo jaa,
 
35Hawatasikia humo upuuzi wala uwongo -
 
36Malipo kutoka kwa Mola wako Mlezi, kipawa cha kutosha.
 
37Mola Mlezi wa mbingu na ardhi na vilio baina yao, Arrahman, Mwingi wa rehema; hawamiliki usemi mbele yake!
 
38Siku atakapo simama Roho na Malaika kwa safu. Hawatasema ila Mwingi wa rehema aliye mruhusu, na atasema yaliyo sawa tu.
 
39Hiyo ndiyo Siku ya haki. Basi anaye taka na ashike njia arejee kwa Mola wake Mlezi.
 
40Hakika tumekuhadharisheni adhabu iliyo karibu kufika; Siku ambayo mtu atakapo ona yaliyo tangulizwa na mikono yake; na kafiri atasema: Laiti ningeli kuwa udongo!
 
 
ReadTheQuran.org