Translations Suras
KISWAHILI

68 - AL - QALAM

KWA JINA LA MWENYEZI MUNGU MWINGI WA REHEMA MWENYE KUREHEMU.

 
1Nuun. Naapa kwa kalamu na yale wayaandikayo,
 
2Kwa neema ya Mola wako Mlezi wewe si mwendawazimu.
 
3Na kwa hakika wewe una malipo yasiyo katika.
 
4Na hakika wewe una tabia tukufu.
 
5Karibu utaona, na wao wataona,
 
6Ni nani kati yenu aliye pandwa na wazimu.
 
7Hakika Mola wako Mlezi ndiye Yeye ajuaye zaidi nani aliye ipotea Njia yake, na Yeye ndiye anaye wajua zaidi walio ongoka.
 
8Basi usiwat'ii wanao kadhibisha.
 
9Wanatamani lau unge lainisha ili nao wakulainishie.
 
10Wala usimt'ii kila mwingi wa kuapa wa kudharauliwa,
 
11Mtapitapi, apitaye akifitini,
 
12Mwenye kuzuia kheri, dhaalimu, mwingi wa madhambi,
 
13Mkavu, na juu ya hayo, mshari, amejipachika tu.
 
14Ati kwa kuwa ana mali na watoto!
 
15Anapo somewa Aya zetu, husema: Hizi ni simulizi za uwongo za watu wa zamani!
 
16Tutamtia kovu juu ya pua yake.
 
17Hakika tumewajaribu hawa kama tulivyo wajaribu wale wenye shamba, walipo apa kwamba watayavuna mazao yake itakapo kuwa asubuhi.
 
18Wala hawakusema: Mungu akipenda!
 
19Basi lilitokea tukio juu yake kutoka kwa Mola wako Mlezi, nao wamelala!
 
20Likawa kama usiku wa giza.
 
21Asubuhi wakaitana.
 
22Ya kwamba nendeni kondeni mwenu ikiwa mnataka kuvuna.
 
23Basi walikwenda na huku wakinong'onezana,
 
24Ya kuwa leo hata masikini mmoja asikuingilieni.
 
25Na walikwenda asubuhi, nao wameshikilia azimio hilo.
 
26Basi walipo liona, wakasema: Hakika tumepotea!
 
27Bali tumenyimwa!
 
28Mbora wao akasema: Sikukwambieni, kwa nini hamumtakasi Mwenyezi Mungu?
 
29Wakasema: Ametakasika Mola wetu Mlezi! Hakika sisi tulikuwa wenye kudhulumu.
 
30Basi wakakabiliana kulaumiana wao kwa wao.
 
31Wakasema: Ole wetu! Tulikuwa tumeikiuka mipaka!
 
32Asaa Mola wetu Mlezi akatubadilishia lilio bora kuliko hili. Hakika sisi ni wenye kurejea kwa Mola wetu Mlezi.
 
33Namna hivi yanakuwa mateso, na bila ya shaka mateso ya Akhera ni makubwa zaidi, laiti wangeli jua!
 
34Hakika wachamngu watakuwa na Bustani za neema kwa Mola wao Mlezi.
 
35Kwani tutawafanya Waislamu kama wakosefu?
 
36Mna nini? Mnahukumu vipi?
 
37Au mnacho kitabu ambacho ndani yake mnasoma?
 
38Kuwa mtapata humo mnayo yapenda?
 
39Au mnazo ahadi za viapo juu yetu za kufika Siku ya Kiyama ya kuwa hakika mtapata kila mnayo jihukumia?
 
40Waulize: Ni nani miongoni mwao dhamini wa haya?
 
41Au wanao washirika? Basi wawalete washirika wao wakiwa wanasema kweli.
 
42Siku utakapo wekwa wazi mundi, na wataitwa kusujudu, lakini hawataweza,
 
43Macho yao yatainama chini, fedheha itawafunika. Na hakika walikuwa wakiitwa wasujudu walipo kuwa wazima -
 
44Basi niache na wanao kadhibisha maneno haya! Tutawavutia kidogo kidogo kwa mahali wasipo pajua.
 
45Na ninawapururia muhula; hakika hila zangu ni imara.
 
46Au unawaomba ujira, na wao wanaemewa na gharama hiyo?
 
47Au iko kwao siri, basi wao wanaiandika?
 
48Basi ingojee hukumu ya Mola wako Mlezi, wala usiwe kama mmezwa na samaki, alipo nadi naye kazongwa.
 
49Kama isingeli mfikia neema kutoka kwa Mola wake Mlezi, bila ya shaka angeli tupwa ufukweni naye ni mwenye kulaumiwa.
 
50Lakini Mola wake Mlezi alimteua na akamfanya miongoni mwa watu wema.
 
51Na walio kufuru hukaribia kukutelezesha kwa macho yao, wanapo sikia mawaidha, na wanasema: Hakika yeye ni mwendawazimu.
 
52Na hayakuwa haya, ila ni ukumbusho kwa walimwengu wote.
 
 
ReadTheQuran.org