Translations Suras
KISWAHILI

55 - ARRAH'MAN

KWA JINA LA MWENYEZI MUNGU MWINGI WA REHEMA MWENYE KUREHEMU.

 
1Arrah'man, Mwingi wa Rehema
 
2Amefundisha Qur'ani.
 
3Amemuumba mwanaadamu,
 
4Akamfundisha kubaini.
 
5Jua na mwezi huenda kwa hisabu.
 
6Na mimea yenye kutambaa, na miti, inanyenyekea.
 
7Na mbingu ameziinua, na ameweka mizani,
 
8Ili msidhulumu katika mizani.
 
9Na wekeni mizani kwa haki, wala msipunje katika mizani.
 
10Na ardhi ameiweka kwa ajili ya viumbe.
 
11Humo yamo matunda na mitende yenye mafumba.
 
12Na nafaka zenye makapi, na rehani.
 
13Basi ni ipi katika neema za Mola wenu Mlezi mnayo ikanusha
 
14Amemuumba mtu kwa udongo wa kinamo..
 
15Na akawaumba majini kwa ulimi wa moto.
 
16Basi ni ipi katika neema za Mola wenu Mlezi mnayo ikanusha
 
17Mola Mlezi wa mashariki mbili na wa magharibi mbili.
 
18Basi ni ipi katika neema za Mola wenu Mlezi mnayo ikanusha?
 
19Anaziendesha bahari mbili zikutane;
 
20Baina yao kipo kizuizi, zisiingiliane.
 
21Basi ni ipi katika neema za Mola wenu Mlezi mnayo ikanusha?
 
22Katika hizo bahari mbili zinatoka lulu na marijani.
 
23Basi ni ipi katika neema za Mola wenu Mlezi mnayo ikanusha?
 
24Na ni vyake Yeye hivi viendavyo baharini vilivyo undwa kama vilima.
 
25Basi ni ipi katika neema za Mola wenu Mlezi mnayo ikanusha?
 
26Kila kilioko juu yake kitatoweka.
 
27Na atabakia Mwenyewe Mola wako Mlezi Mwenye utukufu na ukarimu.
 
28Basi ni ipi katika neema za Mola wenu Mlezi mnayo ikanusha?
 
29Vinamwomba Yeye vilivyomo katika mbingu na ardhi. Kila siku Yeye yumo katika mambo.
 
30Basi ni ipi katika neema za Mola wenu Mlezi mnayo ikanusha?
 
31Tutakuhisabuni enyi makundi mawili.
 
32Basi ni ipi katika neema za Mola wenu Mlezi mnayo ikanusha?
 
33Enyi makundi ya majini na watu! Mkiweza kupenya kwenye mbingu na ardhi, basi penyeni! Hamtapenya ila kwa kupewa madaraka.
 
34Basi ni ipi katika neema za Mola wenu Mlezi mnayo ikanusha?
 
35Mtapelekewa muwako wa moto na shaba; wala hamtashinda.
 
36Basi ni ipi katika neema za Mola wenu Mlezi mnayo ikanusha?
 
37Itakapo pasuka mbingu ikawa nyekundu kama mafuta.
 
38Basi ni ipi katika neema za Mola wenu Mlezi mnayo ikanusha?
 
39Siku hiyo hataulizwa dhambi zake mtu wala jini.
 
40Basi ni ipi katika neema za Mola wenu Mlezi mnayo ikanusha?
 
41Watajuulikana wakosefu kwa alama zao, basi watashikwa kwa nywele zao za utosini na kwa miguu.
 
42Basi ni ipi katika neema za Mola wenu Mlezi mnayo ikanusha?
 
43Hii ndiyo Jahannamu ambayo wakosefu wakiikanusha.
 
44Watakuwa wakizunguka baina ya hiyo na maji ya moto yanayo chemka.
 
45Basi ni ipi katika neema za Mola wenu Mlezi mnayo ikanusha?
 
46Na mwenye kuogopa kusimamishwa mbele ya Mola wake Mlezi atapata Bustani mbili.
 
47Basi ni ipi katika neema za Mola wenu Mlezi mnayo ikanusha?
 
48Bustani zenye matawi yaliyo tanda.
 
49Basi ni ipi katika neema za Mola wenu Mlezi mnayo ikanusha?
 
50Ndani yake zimo chemchem mbili zinazo pita.
 
51Basi ni ipi katika neema za Mola wenu Mlezi mnayo ikanusha?
 
52Humo katika kila matunda zimo namna mbili.
 
53Basi ni ipi katika neema za Mola wenu Mlezi mnayo ikanusha?
 
54Wawe wameegemea matandiko yenye bit'ana ya hariri nzito; na matunda ya Bustani hizo yapo karibu.
 
55Basi ni ipi katika neema za Mola wenu Mlezi mnayo ikanusha?
 
56Humo watakuwamo wanawake watulizao macho yao; hajawagusa mtu kabla yao wala jini.
 
57Basi ni ipi katika neema za Mola wenu Mlezi mnayo ikanusha?
 
58Kama kwamba wao ni yakuti na marijani.
 
59Basi ni ipi katika neema za Mola wenu Mlezi mnayo ikanusha.
 
60Ati yaweza kuwa malipo ya ihsani ila ihsani?
 
61Basi ni ipi katika neema za Mola wenu Mlezi mnayo ikanusha?
 
62Na zaidi ya hizo zipo Bustani nyengine mbili.
 
63Basi ni ipi katika neema za Mola wenu Mlezi mnayo ikanusha?
 
64Za kijani kibivu.
 
65Basi ni ipi katika neema za Mola wenu Mlezi mnayo ikanusha?
 
66Na chemchem mbili zinazo furika.
 
67Basi ni ipi katika neema za Mola wenu Mlezi mnayo ikanusha?
 
68Imo humo miti ya matunda, na mitende na mikomamanga.
 
69Basi ni ipi katika neema za Mola wenu Mlezi mnayo ikanusha?
 
70Humo wamo wanawake wema wazuri.
 
71Basi ni ipi katika neema za Mola wenu Mlezi mnayo ikanusha?
 
72Wanawake wazuri wanao tawishwa katika makhema.
 
73Basi ni ipi katika neema za Mola wenu Mlezi mnayo ikanusha?
 
74Hajawagusa mtu wala jini kabla yao.
 
75Basi ni ipi katika neema za Mola wenu Mlezi mnayo ikanusha?
 
76Wameegemea juu ya matakia ya kijani na mazulia mazuri.
 
77Basi ni ipi katika neema za Mola wenu Mlezi mnayo ikanusha?
 
78Limetukuka jina la Mola wako Mlezi Mwenye utukufu na ukarimu.
 
 
ReadTheQuran.org