Translations Suras
KISWAHILI

54 - AL-QAMAR

KWA JINA LA MWENYEZI MUNGU MWINGI WA REHEMA MWENYE KUREHEMU.

 
1Saa imekaribia, na mwezi umepasuka!
 
2Na wakiona Ishara hugeuka upande na husema: Huu uchawi tu unazidi kuendelea.
 
3Na wamekanusha na wamefuata matamanio yao. Na kila jambo ni lenye kuthibiti.
 
4Na bila ya shaka zimewajia khabari zenye makaripio.
 
5Hikima kaamili; lakini maonyo hayafai kitu!
 
6Basi jiepushe nao. Siku atakapo ita mwitaji kuliendea jambo linalo chusha;
 
7Macho yao yatainama; watatoka makaburini kama nzige walio tawanyika,
 
8Wanamkimbilia mwitaji, na makafiri wanasema: Hii ni siku ngumu.
 
9Kabla yao kaumu ya Nuhu walikanusha; wakamkanusha mja wetu, na wakasema ni mwendawazimu, na akakaripiwa.
 
10Basi akamwomba Mola wake Mlezi akasema: Kwa hakika mimi nimeshindwa, basi ninusuru!
 
11Basi tukaifungua milango ya mbingu kwa maji yanayo miminika.
 
12Na tukazipasua ardhi kwa chemchem, yakakutana maji kwa jambo lilio kadiriwa.
 
13Na tukamchukua kwenye safina ya mbao na kamba.
 
14Ikawa inakwenda kwa nadhari yetu, kuwa ni malipo kwa alivyo kuwa amekanushwa.
 
15Na bila ya shaka tuliiacha iwe ni Ishara. Lakini je, yupo anaye kumbuka?
 
16Basi ilikuwaje adhabu yangu, na maonyo yangu.
 
17Na bila ya shaka Sisi tumeifanya Qur'ani iwe nyepesi kufahamika. Lakini yupo anaye kumbuka?
 
18Kina A'di walikanusha. Basi ilikuwaje adhabu yangu na maonyo yangu?
 
19Hakika Sisi tuliwapelekea upepo wa kimbunga katika siku korofi mfululizo,
 
20Ukiwang'oa watu kama vigogo vya mitende vilio ng'olewa.
 
21Basi ilikuwaje adhabu yangu na maonyo yangu?
 
22Na bila ya shaka Sisi tumeifanya Qur'ani nyepesi kufahamika; lakini yupo anaye kumbuka?
 
23Thamudi waliwakanusha Waonyaji.
 
24Wakasema: Ati tumfuate binaadamu mmoja katika sisi? Basi hivyo sisi tutakuwa katika upotofu na kichaa!
 
25Ni yeye tu aliye teremshiwa huo ukumbusho kati yetu sote? Bali huyu ni mwongo mwenye kiburi!
 
26Kesho watajua ni nani huyo mwongo mwenye kiburi.
 
27Hakika Sisi tutawapelekea ngamia jike ili kuwajaribu, basi watazame tu na ustahamili.
 
28Na waambie kwamba maji yatagawanywa baina yao; kila sehemu ya maji itahudhuriwa na aliye khusika.
 
29Basi wakamwita mtu wao akaja akamchinja.
 
30Basi ilikuwaje adhabu yangu na maonyo yangu!
 
31Hakika Sisi tuliwapelekea ukelele mmoja tu, wakawa kama mabuwa ya kujengea uwa.
 
32Na bila ya shaka Sisi tumeifanya Qur'ani iwe nyepesi kwa kukumbuka, lakini yupo akumbukaye?
 
33Kaumu Lut'i nao waliwakadhibisha Waonyaji.
 
34Hakika Sisi tukawapelekea kimbunga cha vijiwe, isipo kuwa wafuasi wa Lut'i. Hao tuliwaokoa karibu na alfajiri.
 
35Kwa neema inayo toka kwetu. Hivyo ndivyo tumlipavyo anaye shukuru.
 
36Na hakika yeye aliwaonya adhabu yetu; lakini wao waliyatilia shaka hayo maonyo.
 
37Na walimtaka awape wageni wake. Tukayapofua macho yao, na tukawaambia: Onjeni basi adhabu na maonyo yangu!
 
38Na iliwafikia wakati wa asubuhi adhabu yangu ya kuendelea.
 
39Basi onjeni adhabu na maonyo yangu!
 
40Na hakika tumeisahilisha Qur'ani kuikumbuka. Lakini yupo anaye kumbuka?
 
41Na Waonyaji waliwafikia watu wa Firauni.
 
42Walizikadhibisha Ishara zetu zote, nasi tukawashika kama anavyo shika Mwenye nguvu Mwenye uweza.
 
43Je! Makafiri wenu ni bora kuliko hao, au yameandikwa vitabuni kuwa nyinyi hamtiwi makosani?
 
44Au ndio wanasema: Sisi ni wengi tutashinda tu.
 
45Wingi wao huu utashindwa, na wao watasukumwa nyuma.
 
46Bali Saa ya Kiyama ndio miadi yao, na Saa hiyo ni nzito zaidi na chungu zaidi.
 
47Hakika wakosefu wamo katika upotofu na wazimu.
 
48Siku watakapo kokotwa Motoni kifudifudi waambiwe: Onjeni mguso wa Jahannamu!
 
49Kwa hakika Sisi tumekiumba kila kitu kwa kipimo.
 
50Na amri yetu haikuwa ila ni moja tu, kama kupepesa jicho.
 
51Na bila ya shaka tumekwisha waangamiza wenzenu. Lakini yupo anaye kumbuka?
 
52Na kila jambo walilo lifanya limo vitabuni.
 
53Na kila kidogo na kikubwa kimeandikwa.
 
54Hakika wachamngu watakuwa katika Mabustani na mito.
 
55Katika makalio ya haki kwa Mfalme Mwenye uweza.
 
 
ReadTheQuran.org